Dinsdag, Mei 22, 2018

Israel yatumia ndege hatari zaidi ya kivita duniani

 Israel imesema kwamba imetumia ndege za kivita zenye uwezo wa kukwepa mitambo ya rada ambazo zimetengenezewa Marekani kwa mara ya kwanza katika vita.

Ni mara ya kwanza kwa ndege hiyo kutumiwa vitani pahala popote duniani.

Ndege hiyo ilitumiwa katika operesheni ya kijeshi ya jeshi la wanahewa la Marekani.

Mkuu wa jeshi la wanahewa alionyeshapicha ya ndege hizo zikiwa katika anga ya Beirut, Lebanon, na alisema ndege hizo tayari zimetumiwa mara mbili kushambulia, katika maeneo mawili tofauti.

hata hivyo hakusema ni wapi ndege hizo zilitumiwa kutekeleza mashambulizi.

Ndege hizo aina ya F-35 ambazo zimeundwa chini ya mpango ghali zaidi wa zana za kivita duniani zimekosolewa sana kutokana na gharama yake na ufasaha vitani.

Mwaka jana, Waziri wa Ulinzi wa Marekani James Mattis alilazimika kuutetea mradi wa kuunda ndege hizo baada ya Rais Donald Trump kuandika kwenye Twitter akikosoa gharama ya ndege hizo.

Inakadiriwa kwamba ndege moja kama hiyo hugharimu karibu $100m (£74m) kuiunda.

Meja Jenerali Amikam Norkin wa Israel aliwaambia wakuu wa majeshi ya wanahewa kutoka mataifa 20 waliokutana Israel kwamba: "Tunazitumia ndege za F-35 kote katika anga ya Mashariki ya kati na tayari tumeshambulia katika vita maeneo mawili tofauti."

Hakueleza ni wapi walishambulia.

"Unajua, tumeshinda tu Eurovision (shindano ya ustadi katika muziki) majuzi kwa wimbo 'Toy' (kifaa cha kuchezea). Naam, F-35 si toy," alisema.

Israel, taifa pekee kando na Marekani kuwa ndege za aina hiyo, imepokea ndege tisa kati ya 50 aina ya F-35 ambazo imeziagiza.

Taifa hilo limesema linaweza kununua hadi ndege 75.

Israel imezipa ndege hizo jina la Kiebrania la "Adir" (Mkuu).

Ndege hizo zinadaiwa kuwa aina ya F-35A - ambazo zinatumiwa kwa mashambulio ya kawaida ya kupaa na kutua.

Israel ilisema majuzi ilishambulia mitambo ya kijeshi ya Iran nchini Syria.

Marekani imetoa msaada wa kijeshi kwa Israel zaidi ya taifa jingine lolote duniani - kwa sasa unafikia $4bn kwa mwaka - na sheria zake za mauzo ya silaha huhakikisha kwamba Israel bado inasalia na ubabe zaidi ya mataifa mengine Mashariki ya Kati.

  • Ndege hiyo iliundwa na Lockheed Martin na ilipaa kwa mara ya kwanza 2006. Moja ya sababu za ndege hii kupendwa zaidi ni kuweza kutumiwa kwingi. Inaweza kutumiwa na jeshi la wanahewa, wanajeshi wa majini na wanajeshi wa nchi kavu.
  • Kuna aina tatu: ya kupaa kwa njia ya kawaida (A); ya kupaa upesi na kutua kama helikopta (B) naya kupaa kutoka kwa meli za kubeba ndege (C)
  • Ina uwezo wa kukwepa mitambo ya rada
  • Uwezo wake wa kukwepa mitambo ya rada huiwezesha kushambulia ndege za maadui kabla ya kuonekana. Inaweza pia kufyatua ikiwa imeelekea upande wowote.
  • Ina mitambo ya kisasa ya mawasiliano, na marubani wake wanaweza kufuatilia ndege za maadui, kuingilia mitambo ya rada ya maaduni na kuzima mashambulio

Israel imeisifu tena ndege hiyo ya Lockheed Martin F-35.

Ingawa ndio mara ya kwanza kwa Israel kukiri kuitumia, kuna uwezekano kwamba si mara ya kwanza.

Kuna uwezekano iliitumia Januari mwaka jana.

Marekani imewekeza zaidi katika mradi huo unaotarajiwa kuendelea hadi mwaka 2070 na kugharimu karibu $1.5tn kufikia wakati huo.




mubashara blog +255753121916

Geen opmerkings nie:

Plaas 'n opmerking