Sondag, Februarie 11, 2018

Vijiji 100 kupata maji ya Ziwa Victoria


WIZARA ya Maji na Umwagiliaji inatekeleza mradi wa maji wa vijiji 100 vilivyopo kandokando ya bomba kuu kutoka Ziwa Victoria hadi Kahama Shinyanga, Bunge limeelezwa.

Kauli hiyo ilitolewa jana na Naibu Waziri wa wizara hiyo, Jumaa Aweso, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Msalala (CCM), Ezekiel Maige.

Katika swali lake, Maige alitaka kujua ni vijiji vingapi kati ya hivyo 100 hadi sasa vimepatiwa maji.

“Je, Serikali itafikisha lini Maji ya Ziwa Victoria katika vijiji vya Mwakazuka, Mwaningi, Kabondo, Ntundu, Busangi, Buchambaga, Nyamigege, Gula, Izuga, Buluma, Matinje na Bubungu,” alihoji Mbunge huyo.

Akijibu swali hilo, Aweso alisema utekelezaji huo unafanywa kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.Alibainisha katika awamu ya kwanza jumla ya vijiji 40 vilivyopo katika Halmashauri za Msalala, Misungwi, Kwimba na Shinyanga vimetambuliwa na ujenzi wa miradi ya maji katika vijiji 33 umekamilika na baadhi ya vijiji vingine vinaendelea na ujenzi.

Aidha, Aweso alisema vijiji vilivyotajwa na Mbunge ni miongoni mwa 100 vilivyotambuliwa na tayari Halmashauri ya Msalala imekamilisha usanifu wa kina kwenye vijiji ya Ntundu, Busangi, Nyamigege, Gula, Ntobo, Masabi na Chela.

Alisema pia vijiji vya Mwakazuka, Kabondo na Izuga zabuni zake zimeshatangazwa na Kashwasa na tayari mkandarasi amepatikana.

Alisema zaidi kuwa vijiji vya Mwaningi, Buchambaga, Buluma, Matinje na Bubungu vipo katika hatua za awali za utekelezaji.

Kadhalika, Aweso alisema serikali itaendelea kutenga na kutoa fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi katika vijiji vinavyoendelea na vilivyobaki kulingana na Bajeti iliyotengwa.


Chrispiny kalinga blog

Geen opmerkings nie:

Plaas 'n opmerking